|
Tarehe 10 Muharram (Ashura)
Kimeandikwa Na:
Sayyid Murtaza Rizvi
Imam Hussein
(a.s.) na watu wake wenye kumcha Mungu walipigana kishujaa, kuulinda
Uislam na kuitetea “La ilaha Illa llah” hadi tone lao la mwisho
la damu. Wasia aliouandika Imam Hussein (a.s.) alipokua akiondoka
Madina ni “Mimi siondoki hapa Madina kwa sababu ya jeuri au kidunia bali
nafuata njia ya babu yangu Mtume Mtukufu Muhammad (s.a.w.w.) na njia ya
baba yangu Imam Ali (a.s.) ya kuamrisha mema na kukataza maovu”.
Hatimaye
Imam Hussein (a.s.) na watu wake walizingirwa Karbala na kunyimwa maji
kwa siku 3. Tarehe 10 Muharram ni siku ya Ashura ni siku kubwa ya
huzuni, tukiwakumbuka Mashujaa hawa 72 wakiwemo mzee wa miaka 85 hadi
mtoto mchanga wa miezi sita, wakiwemo waafrika, kwa ushujaa mkubwa
waliouonyesha kwa kulinda Dini dhidi ya majeshi ya kidhalim yenye watu
32,000.
Imam Hussein
(a.s.) na watu wake waliuwawa pamoja na mwanawe wa miezi sita. Jeshi la
Yazidi halikuridhika bali walichoma moto mahema ya wanawake watukufu wa
nyumba ya Mtume (s.a.w.w.) na kuchukuliwa Syiria kama mateka wa vitani.
Qur’an
tukufu inasema Mbingu na Ardhi hazikuwalilia watu waovu na wala
hawakupewa muda wa kurejea Duniani. Dhukhan 29 Aya hii inaonyesha
kwamba Mbingu na Ardhi haziwalilii watu waovu bali huwalilia watu wema
kama ilivyopokewa na Sahaba Yazid Ibn Abi Ziyad aliposema: “Alipouliwa
Imam Hussein (a.s.) Mbingu zilipiga wekundu kwa muda wa miezi minne na
kusema kuwa wekundu wake ndio kulia kwake.” Rejea: (Tafsir Ibn Kathir
J. 4, Uk. 155. na Duurul Manthur J. 7 Uk. 412 – 413.).
Msimamo wa
Imam Hussein (a.s.) ungali hai na mhanga aliojitolea umo ndani ya nyoyo
za Waumini ulimwenguni kote. Haya ni malipo ya watu hawa kwa Mtume wao
aliyeleta Dini na Ustaarabu. Jazaa yao ni kuwaua wajukuu zake.
Wameipinga Qur’ani (42:23) isemayo “waambie siwataki malipo yoyote juu
ya (Utume niliokuja nao) ila mapenzi juu ya Aqraba wangu.”
Tumempenda
Mtume (s.a.w.w.) basi lazima tuwapende anaowapenda yeye sio kuwaua. Na
mwisho Mtume (s.a.w.w.) aliusia:- Mimi nawaachia nyinyi makhalifa
wawili: Kitabu cha Mwenyezi Mungu (s.w.t.) na watu wa nyumba yangu, na
kwamba mkishikamana navyo kamwe hamtapotea baada yangu. Rejea: (Musnadi
Ahmad J. 5, Uk. 189.).
|