|
HOTUBA YA MUHESHIMIWA AL-ALLAMAH AL-QADHI AS-SAYYID OMAR IBN AHMAD IBN
SUMAIT AL-ALAWI. ALIYOITOA KATIKA UFUNGUZI WA HAFLA YA KUMBUKUMBU YA
MAUAJI ALIYOFANYIWA IMAM HUSAIN (A.S.) KUMBUKUMBU HIYO ILIFANYIKA MJINI
ZANZIBAR TAREHE 21 MUHARRAM 1361 A.H SAWA NA TAREHE 8 FEBRUARY 1942
Kila sifa njema ni zake Mwenyezi Mungu, na tunaziomba rehma na amani
zake zimshukie Mtume Muaminifu, na ziwashukie watu wa nyumba yake,
Masahaba zake na wafuasi wake wema.
Ama baada ya shukurani na salamu, Mwaka wa sitini na moja B.H. ndani ya
mwezi kama huu, Umma wa Kiislamu uliingia khofu na mila yake nayo
ilitetereka na kuingia dosari. Uongozi wa Umma ukabadilika baada ya
kuuawa kwa kipenzi cha waumini na bwana na mashahidi Husain mwana wa
Imam Ali ibn Abi Talib r.a
Usiku huu wa leo ni mara ya kwanza katika Historia kwa Mashia
Ithnaasharia wa hapa Zanzibar kuadhimisha karne ya kumi na tatu tangu
tukio hilo baya lilipotokea. Na ni kwa mara ya kwanza pia wao kuwaalika
ndugu zao miongoni mwa Waislamu wa mji huu ili washirikiane nao katika
makusudio haya matukufu, kama ambavyo mimi binafsi wameniomba nizungumze
japo kidogo kumuhusu bwana wetu Husain a.s. Kwa hakika mimi nimejizuwia
kuzungumzia tukio hili kama lilivyo kwa ufafanuzi kutokana na mazingira
ya kihistoria yaliyonilazimisha kufanya hivyo. Kwa upande wangu
nimechagua kukubainishieni wale watu walioutendea uovu Uislamu na Mtume
wa Uislamu pamoja na Husain ambaye ni kipenzi cha Mtume s.a.w.
Hapana shaka kwamba watu hao waliwanyanganya watu wa nyumba ya Mtume
s.a.w nguvu na uwezo wa kuhukumu pale (watu hao) walipojipatia wafuasi
wengi duniani na wafuasi wao wakawa wengi. Si hivyo tu bali
waliwahamasisha watu mhamasisho uliopelekea watu wa nyumba ya Mtume
s.a.w na wafuasi wao watambulikane kwa jina la Mashia, kitu ambacho siyo
cha ajabu kwani waislamu wengi ni Mashia (wafuasi) wa nyumba ya Mtume
s.a.w na hujisikia uchungu kutokana na misiba iliyowafika.
Hebu msikilize Imam Al- Busari anasema. "Mashahidi wawili
hawanisahaulishi siku ya Karbala kutokana na msiba uliowapata. Basi
tafadhali walilie kiasi unachoweza.
Nitakutoshelezeni Masikio yenu baada ya kusikia usemi huu kwamba, Sababu
zilizopelekea mashia wa nyumba ya Bw. Mtume s.a.w wawe wengi ni dhulma,
ujeuri na mateso yaliyowafika. Kwa hakika mnyonge hata akawa mnyonge
vipi lakini hawezi kukosa watu wa kumtetea kila mahali.
Amma chanzo cha Ushia na sababu za kudhihiri kwake kilianzia kile
kipindi cha mwaka wa thelathini na tano hijiriyyah wakati Banu Umayyah
wliposimama kupora ukhalifa kutoka kwa Bani Hashim wa kutaka kuupokonya
toka mikononi mwa Imam Ali (k.w).
Matokeo ya hali hiyo ni kuvunjika kwa umoja wa Waislamu na kuanguka kwa
mahusiano ya kidugu yaliyokuwepo miongoni mwao.
Mimi naamini ninyi hamna haja nikwambieni kwamba, "Udugu ndiyo msingi
uliojenga umoja wa Waislamu kiasi kwamba mambo yao waliheshimika
ulimwenguni na nguvu zao ziliimarika na kamwe unyonge haukuwasogelea
isipokuwa baada ya kuukosa umoja huo ambao mara nyingi sana bwana Mtume
s.a.w. aliusisitiza mno katika maneno yake.
Mpaka hapa inapasa nihitimishe maneno yangu na sote tumuelekee
Mwenyezi Mungu tukaugonge mlango wa mema yake na ukarimu wake ili
awarudishie umoja wa Waislamu kama ulivyokuwa hapo awali, na amlinde
mfalme wetu Maulana Sayyid Khalifa ibn Habibu, kisha ampe umri mrefu
pamoja na hekima na tawfiq katika shughuli zake zote.
Wasalam alaikum warahmatullahi wabarakatuh.
|